Tetesi

Simba na Yanga Zapewa Kiungo wa Congo Bure Kabisa

Sambaza....

Kiungo mshambuliaji Fabrice Ngoma ameachana na klabu yake ya Al Hilal na sasa ni mchezaji huru hivyo anaweza kupatikana kwa vilabu  vya Simba na Yanga bure kabisa.

Kiungo mwenye kariba ya juu sana Afrika alijiunga na wababe hao wa Sudan baada ya kuvutiwa na mradi Mcongo mwenzie Florent Ibenge baada ya kudumu kwenye Ligi ya UAE Pro.

Licha ya kuanza vyema kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, hatimaye walishindwa kuvuka makundi kwa tofauti ya mabao huku washindi Al Ahly na Mamelodi Sundowns wakisonga mbele kutoka Kundi B.

Kiungo wa Al Hilal Fabrice Ngoma (katikati) akimiliki mpira mbele ya wachezaji wa  timu pinzani.

Ngoma alionyesha kiwango kizuri msimu huu, akiwa pia na miaka mitatu aliyoitumikia Raja Athletic Club ambapo alishinda Botola Pro na Kombe la Shirikisho la Afrika, lakini hali ya hivi karibuni ya kukosekana kwa utulivu iliyoibuka nchini Sudan ambayo imesimamisha mpira wa miguu kumesababisha wachezaji kadhaa kukimbia nchi hiyo.

Mchezaji na klabu wamefikia makubaliano ya kuachana mara moja ili mchezaji huyo aendelee na soka lake sehemu nyingine, akiachana na mkataba mnono wa miaka mitatu. “Ninaweza kuthibitisha kuwa tunaondoka Al Hilal. Klabu imekuwa nzuri na wasimamizi wote hawana hata neno moja baya,” mwakilishi wake Faustino Mukandila wa BSM Foot alithibitisha kwa iDiski Times. “Kwa bahati mbaya, vita vinafanya kuwa haiwezekani kwa Fabrice kuendelea katika hali kama hiyo.

“Tunataka kuwashukuru watu wa Sudan kwa ukarimu wao na tunawatakia maisha bora ya baadaye.” Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 sasa anaweza kujiunga na klabu yoyote anatakayoichagua kama mchezaji huru na hatarajiwi kukosa timu Afrika.

Fabrice Ngoma (katikati) wakati yupo AS Vita

Fabrice Ngoma amekua akizivutia klabu za hapa nchini kwa nyakati tofauti kutokana na uwezo wake mkubwa japo mara kadhaa Simba na Yanga zimekua zikishindwa kutokana na dau lake kubwa. Sasa ni wazi Mcongo huyo anaweza kuzirudisha vitani tena timu hizi katika dirisha litakalofunguliwa mapema msimu huu wa usajili.

Simba wanamfahamu vizuri Ngoma kwani licha ya kukutana nae katika mchezo wa kirafiki mwaka huu kati ya Al Hilal na Simba lakini pia alikuwepo katika kipigo walichopata kutoka AS Vita cha mabao matano kwa sifuri katika Ligi ya mabingwa Afrika mwaka 2019.

Sambaza....