Ligi Kuu

Baleke Awatungua Tena Ihefu, Simba Yaweka Rekodi Mbeya

Sambaza....

Mshambuliaji wa Simba Jean Baleke ameendeleza ubabe wake mbele ya “Mbongo Maji” Ihefu baada ya kuwafunga tena na kuipa ushindi timu yake ya Simba katika mchezo wa ugenini.

Ikiwa ugenini Mbeya Mbarali katika Dimba la ugenini la Ihefu Simba imefanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao mawili kwa sifuri huku magoli yote yakifungwa na mshambuliaji wake Mcongo Jean Baleke. 

 

Mchezo ulikua mgumu na wa kasi ya hali ya juu huku Ihefu wakicheza vyema katika dakika za mwanzoni na kufanikiwa kutengeneza mashambulizi kadhaa ambayo yalizuiliwa kwa ustadi mkubwa na mlinda mlango namba tatu wa Simba Ally Salim aliyeanza langoni leo. 

Mabadiliko ya kumtoa Ismael Sawadogo na kuingia kwa Nasorro Kapama kulilifanya eneo la kiungo kutulia na Simba kurudi mchezoni na kuuufanya mchezo kuwa wa kushambuliana zamu kwa zamu.

Kipindi cha pili Simba walirudi kwa nguvu zaidi huku mabadiliko ya kumtoa Habibu Kyombo na kumuingiza John Bocco kuzaa matunda kwani ndio kipindi ambacho Simba walicheza vyema na kuuchua mchezo na kupekelea kupata mabao mawili yaliyofungwa na Jean Baleke katika dakika ya 84 na 87.

Jean Baleke akimpiga chenga mlinzi wa Ihefu Nicholaus Wadada.

Kwa ushindi huo Simba katika uwanja wa nyumbani wa Ihefu unaifanya kuwa timu pekee katika timu nne bora katika Ligi kupata ushindi uwanjani hapo kwani Yanga walifunga, Azam nao walipoteza huku Singida Big Stars pekee ndio walipata sare.

Pia kwa upande wa nyota Jean Baleke yeye amefanikiwa kuwafunga mabao matano katika michezo miwili mfululizo ndani ya siku nne kwani alifanikiwa kufunga mabao matatu “hatrick” katika mchezo wa FA na leo amefunga mabao mawili katika mchezo wa Ligi Kuu.

Kwa ushindi huo Simba inafikisha alama  60 wakiendelea kusalia nafasi ya pili nyuma ya Yanga wenye alama 65 ambao watashuka dimbani kesho dhidi ya Kagera Sugar.

 

Sambaza....