Amunike
Blog

Ajib hana thamani ya kuongeza timu ya taifa.

Sambaza....

Kocha mkuu wa timu ya taifa Emmanuel Amunike leo hii amezungumza na waandishi wa habari kwa mara ya mwisho kabla hajasafiri na timu ya taifa kwenda Misri.

Emmanuel Amunike amedhibitisha kuwaacha baadhi ya wachezaji kama Ibrahim Ajib, Shomari Kapombe, Lyanda, Kennedy, Jonas Mkude.

” Tuliita wachezaji 39, lakini hatuwezi kwenda na wachezaji wote 39. Tutaondoka na wachezaji 32 pamoja na vijana wawili Kelvin John na Boniphace kwa ajili ya kizazi kijacho”.

“Ndani ya hawa wachezaji 32 kuna wengine wataendelea na wengine hawatoendelea,mwamko ni mkubwa kila mchezaji anapigana na kutaka kuwa sehemu ya hili tukio”.

Ibrahim Ajib

“Tunajiamini, siku zote ukitaka kufanikiwa kwenye maisha unatakiwa ujiamini na uwe na nidhamu”.

“Tunaenda Misri tutakuwa na mchezo wa kirafiki na Misri pamoja na Zimbabwe, baada ya hapo tutapata wachezaji 23 ambao tutaenda nao Afcon”.

“Tunashukuru kwa kutuunga mkono, haikuwa rahisi , kila safari ina changamoto yake ila inategemeana na unavyoziangalia kuzikabili hizo changamoto”.

” Tunaenda kupigana Misri, hii itakuwa nafasi kwa sisi kuitangaza nchi, kuwatangaza wachezaji wetu pia kuwatangaza na nyie waandishi wa habari kwa sababu itawapa nafasi ya kujenga uhusiano na waandishi wa habari wa nje, asanteni kwa kutuunga mkono na ninatumaini mtaendelea kutuunga mkono”.

Kuhusu kuachwa kwa baadhi ya wachezaji, Emmanuel Amunike amedai kuwa mchezaji anatakiwa anishawishi.

“Haijalishi unacheza nje, kama mchezaji unatakiwa unishawishi mimi kama mchezaji, unapoacha kunishawishi mimi kama kocha siwezi kukuchagua”.

“Nahitaji wachezaji bora ambao wanaweza kuisaidia timu , mmekaa miaka 39 bila kwenda Afcon. Miaka 39 ni namba tu, ila kama tutajiamini sisi tunaweza kufanya vizuri, kwangu mimi haijalishi mchezaji katoka wapi, ninachoangalia kwangu ni kipi huyu mchezaji anaweza kukitoa kwenye timu, thamani ipi ambayo mchezaji anaiweka kwenye timu”

“Uwezo wa wachezaji walioachwa hakunishawishi mimi kama kocha, mimi siangalii mchezaji huyu ni nani awe kaka yangu au dada yangu, ninachoangalia ni kipi mchezaji anaweza kutoa kwenye timu”

“Natakiwa niwe mkweli na maamuzi yangu, najua kila mtu anaweza akawa na mapendekezo yake kwa mchezaji fulani lakini kwa kwangu mimi kama kocha kila mchezaji ni muhimu”.

“Kwangu mimi kama hujitumi hatopata nafasi, kama huna nidhamu hautokuwa na nafasi ya kucheza kwenye timu yangu, nidhamu ni funguo ya mafanikio.”

“Ningekuwa sina nidhamu nisingefika hatua ya kucheza Barcelona. Sisi kama Watanzania tunatakiwa tubadilishe mitazamo yetu”

“Tunakuwa wakubwa, tumefuzu Afcon, nimekuwa nikisema kila siku mimi ni Mwafrika mwenzenu. Nisipowaambia ukweli hakuna atakayekuja kuwaambia ukweli, tuwaamini hawa wachezaji tulionao. Hata hao waliochaguliwa ni Watanzania”.

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x