Blog

Kuna siku Emmanuel Okwi atajengewa sanamu!

Sambaza....

Huyu ndiye mchezaji pekee ambaye amefanikiwa sana kujipenyeza katikati ya mioyo ya WanaSimba.

Utawaambia nini wakakuelewa WanaSimba kuhusiana na Emmanuel Okwi?, hapana shaka huwezi kuwaambia chochote kibaya na wakakuelewa.

Kwao wao Emmanuel Okwi ni malaika, hajawahi kuwakosea hata siku moja. Hajawahi kuwaudhi hata siku moja.

Hata kipindi ambacho alienda kwa mahasimu wao Yanga hakufanya kosa kwa Simba hata kidogo, hawakumwadhibu kabisa.

Waliamini yuko Yanga kimwili pekee tu ila moyo wake wote ulikuwa katika mji wa Msimbazi katika klabu ya Simba.

Hawakuamini kaama anàweza akafanya vizuri akiwa na jezi ya njano na kijani. Hakutaka kabisa kuamini kwenye hilo.

Okwi ni Mchezaji pekee Ligi Kuu Tanzania aliyefunga bao nyingi zaidi ndani ya Mwezi mmoja, amefunga bao Saba.

Imani yao ilibaki moja tu moyoni mwao kuwa Emmanuel Okwi alizaliwa kwa ajili ya kucheza Simba tu na siyo klabu nyingine.

Emmanuel Okwi alizaliwa kwa ajili ya kuwapa furaha mashabiki wa klabu ya Simba tu na siyo klabu nyingine yoyote duniani.

Ndiyo maana alishindwa kufanya chochote kizuri akiwa katika mitaa ya jangwani. Mitaa yenye rangi ya njano na kijani.

Yanga walipoteza hela yao tu kumsajii Emmanuel Okwi. Hawakunufaika kabisa na ujio wa Emmanuel Okwi. Kwa kifupi walipata hasara.

Lakini aliporudi Simba, Emmanuel Okwi makucha yake yalikuwa makali sana. Aliweza kuwinda kila aina ya mawindo tena kwa mafanikio makubwa.

Kwa kifupi ikawa kama amerudi kwenye ardhi ya nyumbani, ardhi ambayo alikuwa anaipigania kwa jasho la damu.

Okwi katika mechi dhidi ya JS Saoura

Ardhi ambayo wazazi wake wapo, ndugu zake wanaishi hapo , kitovu chake kilizikwa pale na hata mwanamke wake wa ndoto yupo pale.

Utaachaje kucheza kwa moyo katika mazingira hayo?, na kizuri zaidi mazingira yalikuwa yanamweka kuonekana kama mfalame wa falme ya Msimbazi?

Mazingira ambayo hajawahi kuyapata sehemu yoyote ile, hata alipoenda ulaya hakufanya vizuri. Hakuwiki, hakuwa na uwezo wa kuwinda sana.

Hakuwa na makali, hakuweza kuheshimika kama ambavyo huwa anaheshimika katika ufalme wa nchi ya Msimbazi.

Sehemu ambayo hucheza kwa moyo wote. Sehemu ambayo huipigania timu kama timu ya baba yake. Sehemu ambayo hufanya kila awezalo ili timu ishinde.

Ndiyo maana kwenye ushindi wa kwanza wa ligi ya mabingwa barani Afrika yeye alionekana ndiye mwenye timu.

Alionekana ndiye mwenye uchungu na timu. Ndiye ambaye alionekana ana nia ya ushindi kuzidi mtu yeyote uwanjani.

Alipigana sana , hakuchoka hata sehemu ambayo alionekana yuko peke yake hakuruhusu kukata tamaa.

Inawezekana Simba kuna wachezaji wengi wamepita tena mwenye majina makubwa lakini Emmanuel Okwi bado atabaki kama mchezaji bora kuwahi kuchezea Simba.

Mchezaji ambaye alikuwa na moyo wa kuichezea Simba. Mchezaji ambaye amesimama kama shabiki mchezaji wa klabu ya Simba.

Anauchungu sana na timu , anacheza sana. Anajituma sana , anatoa pasi za mwisho sana na anafunga sana ili tu ipate mafanikio.

Ni mapema mno kusema Simba msimu huu imepata mafanikio makubwa katika michuano ya Afrika. Lakini kufika hatua ya makundi ni mafanikio makubwa sana.

Okwi Kushoto katika mechi dhidi ya Nkana Fc huko Zambia

Ni mafanikio ambayo yatabaki kwenye kumbukumbu za watu wengi. Wataikumbuka Simba, watawakumbuka wachezaji ambao waliisaidia timu huu.

Kipekee watamkumbuka Emmanuel Okwi, mchezaji ambaye msimu Jana magoli yake 20 ndiyo yaliyomfanya Simba apate nafasi ya kushiriki ligi ya mabingwa barani Afrika.

Emmanuel Okwi ambaye aliwafanya waarabu wajidharau na inawezekana kabisa kwenye michezo mingine ataonesha moto mkali, moto ambao utasababisha tumjengee sanamu pale msimbazi.

Vizazi vyote vitakuja na kuikuta hiyo sanamu. Wataambiwa kuhusu Emmanuel Okwi na watabaki na kumbukumbu kubwa sana kuhusu kipaji chake.

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x