Blog

Kwanini Simba na Yanga ni masikini?

Sambaza....

Pamoja na kuwa na utajiri mkubwa wa mashabiki nchini. Mashabiki ambao wamegeuka kuwa wafuasi wa hizi timu mbili lakini Simba na Yanga zimebaki timu ambazo hazina uwezo wa kifedha.

Kwanini inakuwa hivi ? Zipi sehemu sahihi za vilabu kupata mapato ya kutosha na kuondokana na umasikini ?

HAKI ZA MATANGAZO

Kwa sasa ligi yetu inaoneshwa na Azam Media. Kitu ambacho ni kizuri kwa sababu vilabu hunufaika kutokana na haki ya matangazo.

Lakini kuna vitu viwili ambavyo vinatakiwa kuongezeka kwenye hili. Cha kwanza ni ushindani wa vyombo vya habari vya ndani.

Vyombo vya habari vya ndani vinatakiwa kuleta ushindani kwa Azam Media ili dau la kununua haki za matangazo liongezeke.

Uwezekano wa kuwa na vyombo viwili vya habari vinavyoonesha ligi kuu yetu upo kwa sababu inawezekana. Mfano ligi kuu ya England inaoneshwa na vituo viwili vya ndani ya England ambavyo ni Sky Sports na BT Sports.

BT Sports na Skysports wanalipa pound bilioni 5 kwa ajili ya kununua haki ya matangazo ili waweze kuonesha ligi ndani ya England.


Njia nyingine ya pili ambayo inaweza kutumika hapa nchini ili kuongeza kipato kwa vilabu ni kuuza haki za matangazo kwa vituo vya habari vya nje ya nchi.

Matamasha ya Simba Day na tamasha la wiki ya mwanachi yamekuwa matamasha ambayo yanafuatiliwa sana kwenye nchi za Afrika Mashariki.

Tayari tushaanza kujipenyeza. Tunatakiwa kutumia mipango mikakati mbalimbali ili kuhakikisha tunapata soko la Afrika Mashariki hata kwa nchi moja tu ya Afrika Mashariki.

England imeuza haki za matangazo nchini China kwa vituo vya habari zaidi ya kumi ambapo wanapata pound milioni 560 kwa kuuza haki za matangazo nchini China na vilabu vinanufaika.

Hivo ili kuondoa umasikini wa hivi vilabu viwili lazima tuongeze wigo wa kupata hela nyingi kupitia haki za matangazo.

TIKETI

Hili ni eneo jingine ambalo linaingiza pesa kwa kiasi kikubwa. Uuzaji wetu wa tiketi ni mbovu hapa nchini. Tiketi zinauzwa siku ya mechi tu.

Shabiki akiwa na tiketi yake (Picha: Gumbo)

Hakuna utaratibu wa kuuza tiketi za msimu mzima katika punguzo maalumu kwa mnunuzi. Pia matangazo ya kuuza tiketi huwa hayawekewi mkazo. Vilabu haviwekezi kwenye kutangaza umuhimu wa kununua tiketi kwa mashabiki.

WADHAMINI

Hili ni eneo jingine ambalo halijatazamwa kwa kiasi kikubwa. Machester United kupitia Adidas wanapata pound milioni 75. Pia Manchester United wana udhamini wa kampuni ya magari ya Chevrolet wanayopata pound milioni 50. Kwa kifupi Manchester United wana wadhamini wengi.

Sportpesa anadhamini vilabu kadhaa Ligi kuu

Kwa hapa kwetu hakuna mazingira sahihi ambayo yamewekwa kwa ajili ya kuwa na wadhamini. Klabu inatakiwa kuwa na Benki maalumu , bia maalumu na kadhalika.

Kutokuwa na wadhamini wengi kuna sababisha vilabu hivi kutokuwa na fedha nyingi.

MWANZONI MWA MSIMU

Mwanzoni mwa msimu timu mbalimbali hucheza mechi mbalimbali za kirafiki. Simba na Yanga wana matamasha yao. Matamasha ambayo wanatakiwa kuyatanua.

Wanatakiwa kuyatanuaje? Kwa sababu haya matamasha huchezwa mwanzoni mwa msimu. Kipindi ambacho wanacheza mechi za kujipima nguvu basi matamasha haya yanatakiwa kuanzia mkoani na kilele kifanyike Dar es Salaam.

Simba na Yanga wana mtaji mkubwa sana wa mashabiki kila sehemu. Wakifanya matamasha ya Simba Day au Wiki ya Mwanachi kwenye kila kanda wataingiza pesa.

Tuna kanda tano , kanda ya Ziwa , Kanda ya kati, kanda ya magharibi , kanda ya kusini , kanda ya kaskazini na kanda ya Mashariki. Kwenye makao makuu ya hizi kanda Simba na Yanga wakiwa wanacheza mechi watapata pesa kupitia kiingilio na kuuza jezi. Wakimaliza hapo wanatakiwa kwenda na Zanzibar.

KUUZA WACHEZAJI

Kwa sasa Simba na Yanga hawako kwenye eneo la kushindana na vilabu vikubwa Afrika. Ila ili kujijenga zaidi wanatakiwa kuuza wachezaji kwa vilabu vikubwa Afrika ili kupata fedha nyingi. Fedha ambazo zitawafanya waondokane na umasikini.

MERCHANDISE

Simba na Yanga hawatumii vyema nembo yao kutengeneza bidhaa zenye nembo ya Simba Au Yanga. Bidhaa kama Vikombe , Skafu , Saa nk.

Sambaza....