Blog

Mfaume Mfaume na Idd Pialari ni mpaka mtu afe

Sambaza....

Achana na “Derby” ya kwenye kandanda kati ya Simba na Yanga ambayo ndio maarufu hapa Tanzania na Afrika pia kutokana na upinzani mkubwa wa wawili hao kuna hii “Derby ya kwenye masumbwi “mchezo wa ngumi” kati ya Mabibo na Manzese.

Kuna lile pambano lilifanyika pale Jijini Arusha katika usiku wa funga mwaka lakini halikupata mbabe kwani lilivunjika katika raundi ya kwanza tuu na kufanya kila mtu atoke uwanjani akiwa hajakidhi hamu yake yakumdondosha mwenzake.

Sasa Posh Queen Boxing Promotion [PQBP] inakueletea “King of the Night” pambano la ngumi litakalopigwa Tarehe moja ya mwezi wa tisa mwaka huu katika uwanja wa Uhuru kati ya Mfaume Mfaume na Idd Pialali. Pambano ambalo linadhaminiwa na Mrisho General na Azam Tv.

Katika pambano hilo lililotayarishwa na PQBP litakua ni pambano lenye mkanda na mkataba umesainiwa jana katika viwanja vya Leaders Club na mabondia wote wawili wakishuhudiwa na Rais wa kamisheni ya ngumi TPBRC Chaurembo Palasa.

Katika pambano la awali lililopigwa Jijini Arusha mchezo huo ulishindwa kuendelea baada ya Idd Pialali kupasuka kichwani na hivyo kushindwa kuendelea na mchezo.

Kuelekea pambano hilo Mfaume Mfaume amesemea yaliyopita yamepita na mama yake tayari amempa maelekezo amalize mchezo mapema tuu.

Mfaume Mfaume “Yaliyopita yamepita yaliyotokea siku ya pambano nadhani watu wote waliona waliokua wanaangalia kwenye tv ni uoga tuu hakuna kichwa sasa hivi hakuna kukimbia. Mama Mfaume ameniambia mwanangu kaza buti fanya mazoezi kwa bidii raundi ya tatu mwisho.”

Huyu asipoamkia ICU naacha boxing na Mama Mfaume yule pale ameongea, mimi siongei sana yani kumpiga Pialari ni kama tembo kukanyaga nyanya.”

Mfaume amesema katika mkataba waliousani safari hii lazima pambano limalizike hata kama mtu anapasuka na kutoka damu kama ng’ombe.

“Katika mkataba huu tuliousaini mbele ya rais wa ngumi wa TPBRC Chaurembo Parasa safari hii mtu apasuke, achanike, atoke mtu damu kama ng’ombe afee hakuna kuacha mtu wala kutoka mtu. Asanteni sana,” alisema Mfaume Mfaume.

Aidha kwa upande wa mpinzani wake Idd Pialari yeye amesema haongei sana yupo tayari kufanya kazi huku akiwashukuru mapromota na media.

Idd Pialari akiongea na mashabiki baada ya kusaini mkataba wa pambano lake dhidi ya Mfaume Mfaume

Idd Pialari “Nasemaje mwanaume haongei sana, nasemaje nakwenda kumfunda huyu mtoto. Nashukuru sana promota aliefanya hili pambano na kulitengeneza ili kurudiana, nazishukuru media zote zilizopo hapa kwa kuja na kusapoti.”

Pialari amesema Mfaume sio bondia mzuri na hakuna mtu amempiga hapa Tanzania ni bondia anaepiga vichwa kama kondoo sio mpiganaji.

“Mfaume Mfaume safari hii kazi anayo, nasemaje huyu ni kondoo sio bondia, huyu ni kondoo sasa dawa yake nimeshaipata tayari. Kuna watu wanamtegemea huyu sio bondia kampiga nani hapa Tanzania? Sasa safari hii hamalizi sisi kazi yetu kucheza ngumi sisi mambondia kwasasaivi kazi anayo watu wangu wa Manzese sitawaangusha mtafurahia show,” alisema Idd Pialari.

Sambaza....