Blog

Miaka nane Jangwani ya Kelvin Yondani!

Sambaza....

Ilikua mwanzoni mwa mwezi wa sita mwaka 2012, Tanzania ilipo simama kwa siku kadhaa juu ya sakata la beki kisiki Kelvin Patrick Yondani kutoka Simba Sc na kujiunga Yanga. Ilikua habari ndefu sana, Simba walidai kufanyiwa umafia na Yanga juu ya usajili ule na kuwatuhumu kufanya sajili inayovunja sheria za kimkataba.

Haikua shida kwa mabosi wa Yanga kwani walikua tiyari wameshamuibukia Yondani kwenye kambi ya timu ya taifa na kummwagia pesa ndefu kisha kunasa saini yake. Simba waliumia sana, mioyo ilijawa na huzuni kumkosa beki kisiki ambaye moto wake ulikua ndio unaanza kuwaka kisawasawa.

Huku na huku, pale na kule, rasmi Yondani akawa mali ya Yanga, jezi namba tano mgongoni chuma kikasimama kama beki wa kati, kazi ikaanza kiume. Haikumchukua muda kuthibitisha ubora wake kwa mashabiki wa Jangwani, ngome yao ilikua ya kuaminika huku macho na shauku kuu ikiwa juu ya kijana huyo kutoka Mwanza.

Inyeshe mvua liwake jua, Yondani alikuwa radhi aloe ama aungue ila lango la Yanga libaki salama kwa mapenzi makubwa aliipambania timu hiyo ya wananchi. Utasema alikunywa maji ya jezi za Yanga, kila tone la jasho lake lilipodondoka mashabiki walilifanya kuwa maji ya kunywa, mapenzi yake na mashabiki wa Yanga hayakuelezeka.

Migogoro ni sehemu ya maisha, licha ya kuwa na matatizo mbalimbali ya kinidhamu klabuni hapo lakini hakuchoka kuomba radhi na kuendelea kuwa Mwananchi. Baada ya miaka nane ya ushupavu, upambanaji, upendo na ulinzi thabiti kwenye ngome ya Yanga, wananchi wanaamua kuachana na mlinzi huyu mwenye umri wa miaka 35 sasa.

Mioyo ya watu wa mpira imeumia sana, mashabiki zake wamekasirika, wengi walitegemea baada ya Nadri Haroub Ali “Cannavaro” kuagwa kwa heshima miaka michache ilyopita pale Jangwani alivyostafu basi angefuata Kelvin Patrick Yondani “Cotton”, ila mambo hayakuwa hivyo.

Ni vuguvugu tu la usajili linalowaweka bize mashabiki wa Yanga na kutoonekana kuwa wameumizwa na kuondoka kwa mkongwe huyo lakini roho zao zinawauma na zitawauma daima iwe kwa upendo ama kwa majuto. (Ukweli).

Ifike mahali klabu zetu ziwe na heshima kwa wachezaji wake, haswa wale walioishi nao kwa vipindi vyote vya maisha (shida na raha).

Huu ndio ulikua muda wa kumheshimisha Yondani kwa Wachezaji, mashabiki na wadau wa soka wote nchini, ni muda ambao Yanga ilipaswa kuonesha ukubwa wake kwa kutanabaisha kwanini Yondani amedumu pale kwa miaka mingi namna hio, hii ingeongeza heshima kwa Yanga na kwake Yondani.

Kuvunjika kwa Mpini sio mwisho wa kilimo, Kila lakheri Yondani, Wanamichezo wako nyuma yako na Taifa linakutizama kama kioo chake bora kunako medani ya Soka.


Sambaza....