Benard Morrison
Shirikisho Afrika

Rais Yanga: Tutapambana Morrison Awepo Afrika Kusini

Sambaza....

Kuelekea mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, Rais wa Yanga amesema wanamuhitaji winga wao Benard Morrison katika michezo yote miwili hivyo watapambana awepo kuwatumikia Wananchi.

Benard Morrison amepigwa marufuku kuingia nchini Afrika Kusini kutokana na makosa aliyoyafanya wakati anaitumikia Orlando Pirates wakati huo.

Yanga watakua wageni wa Marumo Gallacts katika mchezo wa marudiano utakaopigwa May 17 nchini Afrika Kusini na tayari Rais wa Yanga amesema “Tunajiandaa kuomba huruma yao. Tayari tumeanza kuwasiliana na ubalozi wa Afrika Kusini na kujaribu kutatua suala hilo,” Rais Hersi aliiambia Kickoff  Magazine

Benard Morrison akiitumikia Orlando Pirates.

Injinia Hersi Said amesema wanajua umuhimu wa Morrison hivyo wapo tayari kufanya lolote linalowezekana ili wapate huduma yao Morrison wakiwa ugenini nchini Afrika Kusini.

“Tuko tayari kufanya kila kitu kuhakikisha kuwa kila kitu kimepangwa na mchezaji atasafiri kwenda Afrika Kusini na tuko tayari kuzingatia masharti yao.” Hersi Said

Ikumbukwe Watani zao Simba walishindwa kumtumia mara mbili Benard Morrison katika michezo yote miwili ya ugenini pale walipokutana na Kaizer Chiefs na Orlando Pirates katika michezo ya Kimataifa kutokana na marufuku hiyo yakutokuingia nchini Afrika Kusini.

Sambaza....