Mabingwa Afrika

Simba ina kila sababu ya kuwashangaza wengi.

Sambaza....

Acha tu, lakini kufungwa kunauma sanaa ! vuta picha Simba SC isingefika fainali mapinduzi cup kisha isinge shina nafasi ya tatu mashindano ya SportPesa hali ya hewa ingekuwaje pale mitaa ya Msimbazi, vipi mashabiki wake?!! We acha tu!

Klabu ya Simba inatupa karata yake nyingine katika muendelezo wa michuano ya klabu bingwa Afrika, jumamosi hii pale nchini Misri kuwavaa National Al Ahly, wakiwa na kumbukumbu ya kupoteza nyumbani kwa AS Vita Club.

Matokeo ya kule Congo yameonekana kushusha morali ya timu kwa kiwango kikubwa, kiasi kwamba mchezo dhidi ya Al Ahly unaonekana ni wa kawaida sana  kwa Simba, kwani wengi wanajua Simba ni lazima tu apoteze.

Mpira haupo hivyo, unaweza ukawa vizuri na bado ukafungwa, pia historia ya Simba kwa timu kama Al Ahly sio mbaya kwahiyo inatia hamasa zaidi na zaidi. Simba ile ya dhidi ya JS Saoura ilikuwa bora zaidi ndio maana iliibuka na ushindi wa 3-0, Simba ile ile ndiyo iliyoshushiwa mvua ya magoli pale Kinshasa.

Unaikumbuka mechi ya Simba dhidi ya Al Masry mwaka 2018 shirikisho Afrika uwanja wa taifa? Ulipigwa mwingi tu na Simba ikalazimishwa sare ya 2-2, ilikuwa ni machi 7, na mvua zilikuwa zimeanza, masika yalitibua hali ya hewa, isingekuwa mvua huenda leo tungeongea mengine pia.

Nakumbuka kwenye mechi hiyo, Simba walianza kivingine kabisa, beki wa kulia wa Simba, Shomari Kapombe akichezeshwa kama kiungo katika mfumo wa 3-5-2, Aishi Manula, Nicholus Gyan, Asante Kwasi, James Kotei, Yusuph Mlipili, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Shomari Kapombe, Emmanuel Okwi, John Boko na Shiza Kichuya walianza.

Simba walianza kupata goli kwa mkwaju wa penati ya Boko dakika ya 10, kisha Mohamed Gomaa akasawazisha dakika ya 11, baadae Masry wakapata goli lingine dakika ya 26 kupitia kwa Ahmed Abdalraof, Okwi akaweka mzani sawia kwa goli la penati dakika ya 74.

Achana na mechi ya kwanza, ile ya marudiano ndiyo inayonipa picha halisi ya kile kitakachoweza kutokea dhidi ya Al Alhly ugenini. Mechi ya pili ya marudiano dhidi ya Masry ilipigwa tarehe 17 mwezi huo huo wa tatu ikiwa ni siku kumi tu baada ya mechi ya kwanza. Simba iliwashangaza wengi, ilitoa sare ya kutofungana  0-0 huku dakika za mwishoni, Masry wakiomba mpira uishe haraka.

Chini ya Mfaransa Pierre lechantre na Masoud Djuma kama kocha msaidizi, Al Masri walivuka hatua hiyo kwa ushindi wa faida ya goli la ugenini.

Kikosi kilichoivaa Al Masri ndicho hicho hicho kitakachoivaa Al Ahly, kina mabadiliko kidogo kwa baadhi ya wachezaji kama Laudit Mavugo, Said Mohamed, Said Ndemla, na Mwinyi Kazimoto ambao hawapo na kikosi kwa sasa, bila kusahau mabadiliko ya benchi la ufundi, sasa liko chini ya Mbelgiji, Patrick Aussems.

Ukiitazama Simba ya sasa chini ya Aussems, kuna vitu imevibadili kuanzia  kwenye mfumo hadi falsafa. Sasa Simba inacheza “total football” yaani utamkuta Boko yuko katika jukumu la ulinzi, utamkuta Clatus Chama na Mkude wanafunga magoli. Simba ya Lechantre ilikuwa inashambulia kupitia pembeni, hapo utamuona Shomari Kapombe, na Asante Kwasi waking’aa, Simba hiyo ilikuwa inahitaji watu wa kupitia pembeni wakiwa na kasi kubwa, ndio maana Shiza kichuya wa Lechantre ni muhimu zaidi kuliko Kichuya wa Aussems hii yote ni kwa sababu ya falsafa ya mwalimu.

Tuiangalia Simba sasa, kipindi cha Aussems na matokeo ya kimataifa, hapo ndipo utajua mpira ni sayansi na sayansi ni “kukinzani kifalsafa” hii namaanisha, kipindi Aussems anajiandaa na aina Fulani ya Game plan, ndio kwanza Frolent Ibenge naye anaweka mitego yake ya kumlaza kwa 5-0 pale Kinshasa.

Kucheza ugenini, tena na klabu kubwa lazima uonyeshe nidhamu, nidhamu yenyewe sio “kupaki basi” bali kukaba na kushambulia kwa nidhamu, kujituma, kila mchezaji lazima ajitahidi kufika eneo husika, kwa wakati husika” Accuracy” lazima iwe kubwa kwa  kila mchezaji.

Kilichomuangusha Aussems kwenye mechi dhidi ya AS Club Vita ni kuwa na ‘game plan’ isiyofiti kwa wachezaji wake. Kumbuka Simba ilianza na viungo wakabaji watatu, Jonas Mkude, Mzamiru Yassin na James Kotei huku Chama akionekana kupewa jukumu la kupenyeza pasi kwa washambuliaji wa kati, Okwi na Meddie kagere.

Tofauti kubwa iliyoonekana ni Simba kutaka kumiliki mpira, lakini walikuwa taratibu “Slow” sana, kuanzia katika eneo lao na hata eneo la mpinzani. Chama na Mzamiru walionekana kuchelewesha mipira, kutokuwa na “Accuracy” iliyohitajika na mwalimu na aina ya mechi kiujumla, ndio sababu ya Simba kula 5.

Munganga, Ngoma, Kasengu na Muzinga, walikuwa na kasi hasa wakifika nusu ya uwanja, huku wakipiga pasi ndefu. Kasi ya Makusu na Kisinda iliwazidi mabeki wa Simba kama Paschal Wawa na Juuko Mursheed. Physique ya wachezaji wa Simba ilionekana kuwa dhaifu kiasi kwamba, Mohamed Hussein  hakuwa na uwezo wa ku-Overlap kupitia kwa Djuma Shabani kutokana na physique yake kuwa hafifu kulinganisha na anayempita.

Mipira ya 50 kwa 50 wachezaji wa Simba walikuwa wakiishia kupokonywa tu. Lau Shungu ni kocha msaidizi wa AS Club Vita pia alishawahi kuifundisha Yanga SC miaka ya 99  anasema kuwa, Simba ni timu nzuri lakini wanacheza mpira laini “Soft Football”.

“tumeangalia mechi za Simba, dhidi ya Nkana ya Zambia…. Ni rahisi sana kugundua udhaifu wao na kuwafunga..”

“Simba ni timu nzuri wanacheza mpira lakini mpira wanaocheza sio wa kasi, wanapiga pasi zisizo na faida na timu, wanapoteza pasi na muda mwingi kwa kupiga pasi fupi fupi, sisi tunarudi nyuma, tukipata mpira tunapiga mbele… wanachokosa ni Spidi ya kwenda mbele…..”                                                                                                                 “Tunafanya mazoezi ya nguvu sana, tunawaweka sawa wachezaji kisaikolojia waamini kuwa maisha yao ni soka” aliongeza Lau Shungu.

Maneno ya kocha huyo yanadhihirisha wazi kabisa kuwa Simba haikuwa na Physique kubwa na ilikosa kasi wakati wa kupiga pasi, Chama alikuwa anakaa na mpira zaidi ya sekunde 25 hii inawafanya maadui kujipanga ndio maana Aussems alimtoa baada ya kipindi cha kwanza. Alijua tatizo ni yeye na Mzamiru.

Katika kusawazisha hilo, nimeitazama Simba katika mashindano ya Sportpesa, katika mechi zake dhidi ya AFC Leopard, Bandari FC na dhidi ya Mbao FC.

Katika mchezo dhidi ya Leopard ya Kenya, Simba walionyesha kushindwa kuwa na kasi inayohitajika, juhudi binafsi za Okwi zilionekana kuibeba Simba, tatizo la Congo lilionekana halikutatuliwa, kasi ya Simba ilikuwa ndogo kuanzia nyuma hadi katika nusu ya uwanja.

Mchezo dhidi ya Bandari, Simba ililala kwa goli 2-1, kipindi cha kwanza kinamalizika, Simba ilikuwa mbele kwa goli 1 la Meddie Kagere, lakini aina ya Mpira waliokuwa wakicheza ulikuwa Soft mno, Simba ilikuwa inapiga pasi zisizo na faida, yaani Hassan Dilunga alikuwa hana “Accuracy” kwa vitu vingi.

Kocha wa Bandari alionekana  kuisoma Simba ndio maana hata kipindi cha pili, waliingia wakiwa wanajiamini  kwa kupiga pasi ndefu na kuongeza kasi wakiwa eneo la nusu ya uwanja, walizidisha presha langoni kwa Simba, hatimaye walipata ushindi.

Katika mechi ya mwisho, ya kutafuta mshindi wa tatu dhidi ya Mbao FC, Simba walionekana kuimarika katika kipengele cha kasi, walionekana kuwa na kasi maradufu katika eneo la kati na eneo la pembeni hasa beki ya kulia, Zana Oumary Coulibaly. Lakini hata hivyo viungo wengi wa Simba sio wapigaji nje ya 18, yaani leo hii Chama angekuwa na U-Ndemla, basi Simba isingelazimika kupata ushindi wa penati.

Al Ahly Vs Simba SC.

Itakuwa ni mechi ngumu kwa Simba, ukizingatia Saikolojia ya Wachezaji na Mashabiki imesha vurugika kwa sasa, lakini mbinu “game plan” ndiyo itakayoamua mshindi katika mchezo huu.

Sitarajii mabadiliko ya Game Plan ya Patrick Aussems katika mechi dhidi ya Al Ahly ikiwa ni tofauti na ile aliyoitumia dhidi ya AS Club Vita ugenini, kwanza ni kutokana na kocha mwenyewe kuwa ‘king’ang’anizi’ yaani akishikilia mchezaji Fulani basi ni huyo huyo milele, na hata mfumo wake usitarajie kubadilika kirahisi, ukitaka kubaini hilo muangalie katika mechi zake dhidi ya Nkana ugenini na nyumbani, Mbabane Swallows pia nyumbani na ugenini, pili ndio aina sahihi ya game plan ya Ugenini.

Kama Aussems atarekebisha safu yake ya ulinzi na kiungo basi mambo yatakuwa poa sana. Yaani wachezaji lazima wawe na nidhamu ya hali ya juu. Waarabu watakuwa wameshaisoma Simba kwa kiwango kikubwa, bila shaka watashambulia kwa kasi.

Watakuwa wameshajua, Physique ya wachezaji wa Simba ni ndogo, kwahiyo wakitumia nguvu itakuwa ni rahisi kupata ushindi mkubwa nyumbani, bila shaka waatakuwa wanajua adui mkubwa kwa beki ya Simba ni Presha kubwa, yaani kasi ya mashambulizi huwachosha mabeki wa Simba na kupoteza umakini, hivyo wakiongeza kasi eneo la ushambuliaji la Simba watapata chochote kitu.

Itakuwaje kama AL Ahly wakitumia nguvu nyingi na kasi kubwa wakati wa kushambulia? Sawa Simba itafungwa lakini sio goli 5 kama ilivyo kwa AS Club Vita.

Lakini yote ya yote mpira ni sayansi na nina imani kubwa na Kocha wa Simba Aussems, miongoni mwa makocha wakubwa Afrika na kule nchini Ufaransa, nina imani na wachezaji wa Simba, wengi wana uzoefu kama Okwi, Kagere, Chama, Boko, Mkude, Manula na Sergie Wawa.

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x