Robertinho Oliveira
Uhamisho

Uongozi Simba Haudaiwi, Kocha Ajiandae

Sambaza....

Wapwa,  baada ya mchezo ule wa robo fainali ya klabu bingwa kati ya Simba SC dhidi ya Wydad Casablanca msimu ulioisha pale Morocco kwenye uwanja wa Mohamed V moja kati ya vitu ambavyo kocha mkuu wa Simba aliongelea ni usajili.

Hii ilikuwa moja kati ya mechi bora sana ambayo Simba waliicheza kwenye mashindano hayo kuanzia uwanja wa nyumbani mpaka ugenini pale Morocco ila changamoto ya mikwaju ya penati ikawaondoa kwenye mashindano.

Kocha mkuu wa Simba, Roberto Oliveira baada ya mechi ile alifanya mahojiano na Ahmed Ally kupitia Simba APP na miongoni mwa vitu alivyozungumza ni kuwa klabu inapaswa kufanya usajili wa wachezaji Bora kwenye baadhi ya maeneo

Robertinho alihitaji wanapokosekana Shomari Kapombe, Kibu Denis, Clatous Chama, Henock Inonga, Sadio Kanoute, Baleke na wengine Basi upatikane ubora kutoka benchi na kwenda uwanjani kutoa huduma kama wanayotoa hao waliokosekana.

Wachezaji wa Simba katika mchezo wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa walioondoshwa na Wydad Casablanca.

Vizuri. Kila mmoja alikubaliana naye sababu Simba ya msimu uliopita kulikuwa na utofauti mkubwa sana wa ubora kutoka kwa waliopo ndani ya uwanja na waliopo benchi. Hapa Ujumbe ukafika kwa wahusika, nini kikafanyika ?

Simba wamekaa na wamefanya usajili wa wachezaji wapya ambao wana ubora na wanaweza kutoa usaidizi mnzuri kama ambavyo aliomba. Simba imemsajili Che Malone, Miquissone, Ngoma, Onana na Kramo hao ni wachezaji wa viwango vya juu kutoka nje ya nchi.

Che Malone na Onana ni MVP’s kwa walipotoka! Kramo ni mchezaji wa daraja la juu kwa klabu na Ligi aliyotoka ( Asec Mimosas & Ivory Coast )! Fabrice Ngoma ubora wake unafahamika kuanzia AS Vita mpaka pale Al Hilal, Luis Miquissone kama akiwa yule basi sio stori tena lazima atatoa kitu bora sana.

Wachezaji wapya wa Simba.

Simba imefanya usajili Mkubwa sana kazi imebaki kwa Robertinho kuzalisha matokeo bora kupitia maingizo mengi ya wachezaji hao wa nje pamoja na wale wa ndani waliosajiliwa, sidhani kama viongozi wa Simba wanadaiwa kwenye usajili wa msimu huu.

Rahisi! Kilichobaki sasa ni kocha kutengeneza timu imara zaidi kupitia wachezaji waliopo na waliosajiliwa ili kurudisha na kuipa Simba SC mataji waliyopoteza kwa miaka miwili na mafanikio ambayo wameyatafuta kwa muda mrefu.


Sambaza....