Ligi Kuu

Kuna wakati Manara anajing’ata ulimi wake.

Sambaza....

Instagram ndiyo sehemu ambayo watu wengi maarufu hapa nchini kwetu hutumia kuonesha maisha yao binafsi na maisha ya biashara zao. Kwenye dunia hii ya sasa kila kitu ni biashara, na ili ufanikiwe kwenye kila kitu unachokifanya lazima ukifanye kwenye jicho la biashara.

Ndiyo maana Diamond Platnumz aliondokana na dhana ya muziki ni burudani akafikiria namna ya kufanya biashara kwenye muziki na akafanikiwa kwa kiasi kikubwa. Leo hii tunamsifia Mbwana Samatta kwa kile anachokifanya kwa sababu aliamua kuifanya miguu yake iwe duka.

Hakutaka kufungua kibanda cha kuuza nguo , ila mawazo yake yalikuwa kuufanya mguu wake uwe duka linalotembea.

>>>Manara awashukia mashabiki wa ‘mitandaoni’.

Alitembea nalo tena kwa juhudi kubwa kutoka Tanzania mpaka Ubelgiji. Haikujalisha ugumu wa safari yake lakini Cristiano Ronaldo alitembea na miguu yake kutoka Ureno, akaenda England, Hispania ikamkaribisha na duka lake mwisho amelipeleka Italy.

Ndiye mchezaji anayelipwa fedha nyingi na hii ni kwa sababu aliamua kuufanya mpira wa miguu kuwa biashara yake.

Kwa kifupi kila kipaji ambacho mwenyezi Mungu humtunuku mwanadamu yoyote kama kikitumika katika jicho la biashara humnufaisha kwa kiasi kikubwa.

Ndiyo maana kuna jicho la kibiashara katika maisha Haji Manara, ameamua kuendana na mahitaji ya dunia ya sasa.

Anajua ipasavyo kuwa dunia ya sasa ni ya kibiashara na kila kitu ambacho mwanadamu alichonacho anatakiwa kukifanya katika jicho la kibiashara.

Biashara ya Haji Manara iko mdomoni, ameshatambua hilo na anawezekeza muda wake mwingi kukuza biashara yake.

Ndiyo maana hata ukurasa wake wa Instagram unazidi kuwa na watu wengi wanaomfuata na hii ni kwa sababu amewaambiwa kuwa kuna biashara anayoifanya (biashara ya kusema).

Manara(Kulia) na Mo Dewji(Kushoto, Mwekezaji)

Ndiyo maana kuna watu laki nne na elfu hamsini na saba wanaomfuata Instagram kwa minajili ya kupata bidhaa yake anayoizalisha, bidhaa ya uongeaji.

Biadhaa ambayo aliamua yeye mwenyewe kuifanya na kuitafutia Brand Manager wake, mwanamama Beatrice Ndung’u.

Mwanamama ambaye kila uchwao hufanya mahubiri ya namna ya kutumia jina la mtu maarufu kibiashara.

Kumwajiri huyu mwanamke ambaye kwenye ubongo wake kuna mwanga uliofunika giza ilikuwa dalili kubwa kuwa Haji Manara alikuwa ameamua kutumia jina lake kibiashara.

Akili yangu ilitulia na moyo wangu kukubali kuwa Haji Manara ameamua kuishi katika matakwa ya dunia ya leo.

Lakini kuna kitu kimoja anakisahau, pamoja na kwamba dunia ya leo inataka kila kitu kifanyike katika mazingira ya kibiashara, lakini unapoihubiri bidhaa yako unatakiwa uihubiri katika uhalisia wake.

Uhalisia ndiyo hujenga wateja wa dhati wa bidhaa yako. Uhalisia huondoa malalamiko mengi ya wateja wako juu ya bidhaa yako.

Pamoja na kwamba Haji Manara yeye binafsi ni bidhaa lakini muda mwingi hutumia kuihubiri bidhaa ya Simba ambayo ndiyo imemwajiri.

Bidhaa ya Simba imebeba wateja wengi sana, wateja ambao hutamani kusikia maendeleo ya bidhaa yao.

Kitu kizuri kuhusiana na wateja hawa , wenyewe hutaka kusikia ukweli tu kuhusiana na bidhaa wanayoinunua.

Wakati Simba ikiwa Uturuki kwenye maandalizi ya msimu mpya Haji Manara alikuwa anatumia ukurasa wake wa Instagram kuwaaminisha wateja kuhusiana na uimara wa bidhaa ya timu ya Simba.

Aliwaaminisha kuwa kwa maandalizi yale wategemee ubora ambao hawajawahi kukutana nao, hata katika post ya tarehe 27 mwezi wa 7 hakusita kusema msimu huu ataenda na kikombe cha kahawa na haluwa uwanjani.

Ilifika wakati mpaka akaandika tarehe 28 mwezi wa saba mwaka huu kuwa mazoezi ambayo Simba wanafanya ni mazoezi ya kucheza na kina Messi.

Messi ambaye ni mchezaji wa daraja la juu, kauli hii iliwafanya wachezaji wa Simba wajenge picha kubwa.

Picha ambayo ilionesha kuwa hakuna timu hapa nchini inaweza kushindana nayo. Magoli mengi na mpira wa kuvutia ilikuwa kitu cha halali kwao.

Hawakuamini katika ushindi mwembamba kwa sababu timu yao ilikuwa inafanya mazoezi ya kucheza na wachezaji wa daraja la juu duniani.

Ndiyo maana hata baada ya mechi mbili (Mechi ya Simba day na mechi ya ufunguzi wa ligi kuu Tanzania bara dhidi ya Prisons) mashabiki walionekana kutoridhishwa na matokeo ya Simba na hii ni kwa sababu Haji Manara aliwaaminisha kuwa timu yao ilienda Uturuki kufanya mazoezi ya kucheza na kina Lionel Messi.

Leo hii anahangaika kuandika makala yakuwaomba mashabiki wawe na subira na kusahau kuwa aliwaaminisha timu yao kwa sasa imeimarika mpaka kufikia hatua ya kucheza na kina Lionel Messi.

Hapa ndipo ambapo Haji Manara anapouadhibu ulimi wake kila uchwao kwa kuuma kutokana na mambo ya nyumba ambayo anayasema.

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x