Ligi Kuu

Simba na kisasi dhidi ya Hamis Kiiza!

Sambaza....

Kikosi cha Simba kitakua uwanjani leo kiwakaribisha Kagera Sugar katika mchezo wa duru la pili utakaopigwa katika Dimba la Benjamin Mkapa majira ya saa moja jioni.

Katika mchezo wa duru la kwanza Simba iliangukia pua baada ya kukubali kipigo cha bao moja bila lililofungwa na Hamis Kiiza “Diego wa Kampala” katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera.

Katika mchezo wa leo ni muhimu kwa Simba kwa maana mbili, kwanza kabisa ni kulipa kisasi cha mchezo wa raundi ya kwanza kwa goli lililofungwa na mshambuliaji wao wa zamani Kiiza. Lakini pili kuendelea kukusanya alama na kuipa presha Yanga iliyodondosha alama katika michezo mitatu mfululizo.

Tayari Kagera Sugar wamejinasibu kuendeleza palepale walipoishia katika mchezo wa mwisho baina yao, huku Simba wao wakitanabaisha umuhimu wakukusanya alama 3 muhimu.

Simba inashika nafasi ya pili nyuma ya Yanga wakiwa na alama 46 wakishuka dimbani mara 22. Kagera Sugar wao wanashika nafasi ya 6 wakiwa na alama 29 ambapo ushindi wa leo utawapeleka mpaka nafasi ya nne wakiwa sawa na AzamFc. 

Sambaza....