Kelvin John akipongezwa na wenzake
Blog

Nilikuwa namuona Malinzi kwenye miguu ya kina KELVIN JOHN

Sambaza....

Kipi kinakufanya umkumbuke Jamal Malinzi , raisi wa TFF aliyepita ?. Wakati jana niko kwenye uwanja wa Taifa natazama mechi ya Serengeti Boys na Nigeria.

Nilimkumbuka Jamal Malinzi. Ghafla taswira ya mawani yake kwenye paji lake la uso ilikuja kwenye mboni yangu.

Rangi yake nyeusi ilivaa kabisa kwenye akilƙ yangu. Ufahamu wangu ulivaliwa na umbo lake nene kiasi. Alikuwa mwenye siha.

Masikio yangu yakawa yanapitisha sauti ya upole inayoongea taratibu ya Jamal Malinzi. Ghafla picha ya Jamal Malinzi ikaja kwenye ufahamu wangu.

Nikaanza kumfikiria tena muda huu atakuwa anafanyeje ? Hapana alikiwa mahabusu amekaa, akisubiri tarehe ya kesi yake kutajwa(Mungu amtie wepesi kwenye ugumu huu).

Hapana shaka muda huo alikuwa amekaa mbele ya Television akiwatazama vijana wa Serengeti Boys wakicheza dhidi ya Nigeria.

Lazima tu angekuwa anawatazama na kuna wakati alikuwa anatamani ƙkabisa angekuwepo uwanjani kuwatazama kwa ukaribu zaidi kuliko kwenye luninga.

Jamal Malinzi, Rais wa zamani wa TFF

Hii ndiyo faraja yake kwa sasa. Na inawezekana ukiitoa faraja ya familia yake , faraja ya michuano hii ya Afcon na timu hii ya taifa ni ya pili kwa ukubwa kwake.

Inawezekana tunaweza tukawa tumemsahau ƙkabisa kwa sasa. Na inawezekana kuna watu wameshamhukumu kwa sasa na wanamuona kama mkosaji mkubwa.

Na kuna uwezekano mkubwa kuna watu wanamchukia sana kwa sasa kwa sababu tu ya tuhuma ambazo anakabiriana nazo.

Lakini ukweli unabaki pale pale kuwa Jamal Malinzi ana mchango mkubwa kwenye mashindano haya na timu hii mpaka sasa hivi.

Yeye ndiye ambaye alipigana mpaka tukapata nafasi ya kuwa wenyeji wa michuano hii ya Afcon ya vijana waliochini ya umri wa miaka 17.

Yeye ndiye ambaye alipigana ipasavyo kuwaandaa hawa vijana ambao leo hii wanaiwakirisha nchi yetu. Wakati ƙkina Ramadhani Kabwili wakiwa Gabon tulikuwa tunajiuliza ni kizazi kipi kingine ambacho kitaenda Afcon.

Jamal Malinzi alihakikisha tunapata vijana ambao ni mbadala vijana ambao ni imara kwenye michuano hii.

Kwa kushirikiana na kituo cha michezo cha shule ya Alliance , Malinzi aliwakusanya vijana ambao wana umri wa miaka 15 kushuka chini.

Akawaweka pamoja kwa muda mrefu ndani ya shule ya Alliance kule Mwanza. Wamekaa kwa muda wa miaka kuanzia mitatu kwa pamoja.

Kwa ajili tu ya michuano hii ambayo imeanza jana. Hapa ndipo ulikuwa mwanzo wa mimi kuanza kumuona Jamal Malinzi ndani ya miguu ya hawa watoto.

Jamal Malinzi kawafanya wafike hapo walipo kwa matumaini ya kujenga kikosi imara chenye ushindani mkubwa.

Leo hii ukimsifia Kelvin John, au Edmund John unatakiwa usisahau kumsifia Jamal Malinzi katika makuzi yao.

Mtu ambaye alitengeneza njia nzuri ya kuwapata hawa vijana, kuwalea na kuwatunza vizuri kwa ajili ya michuano hii.

Tunaweza kusema Jamal Malinzi aliwapa njia ya kupitia hawa vijana mpaka kufikia hapa walipo.

Wakati kina Yohana Nkomola, Ramadhan Kabwil wakiwa wanatoka Gabon , swali kubwa lilikuwa ni kizazi kipi ambacho kitafuata?

Jamal Malinzi akatuletea kina Kelvin John. Na hapa kuna swali ambalo kina Walliace Karia wanatakiwa wajiulize wakati michuano hii ikiendelea.

Kina Kelvin John watapita , baada ya wao kupita kuna kina nani ambao watakuja kuvaa viatu vyao? Kuna juhudi gani zinafanyika ili kupata wachezaji wengine ili tujenge tabia ya kushiriki mara kwa mara kwenye michuano hii ?

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x