Blog

Zahera alimzika Fei Toto, anamuua Balama

Sambaza....

Ushawahi kuwauliza watu wa Unguja kuhusu Fei Toto? Moja ya swali ambalo watakujibu huku wakiumia ni nafasi gani halisi ambayo Fei Toto huwa anacheza kabla hata hajafika Yanga.

Watakupa jibu huku mioyo yao ikiwa inapata uchungu mkubwa. Kwanini nasema hivi ? Muda huu wanaona Fei Toto kaozeshwa mwanamke asiyempenda.

Kwa vile baba kasema na anamheshimu baba yake inabidi tu afanye kile ambacho baba anataka Ila kiuhalisia Fei Toto hana furaha katika eneo ambalo Lipo.

Eneo ambalo halimuoneshi rangi yake halisi kabisa ambayo wengi wanaijua. Rangi ya kutengeneza nafasi nyingi za magoli, rangi ya kufunga magoli mengi.

Rangi ambayo kwa sasa huwezi kuiona kwa sababu ya ukungu ambao umetanda kuzunguka eneo ambalo yupo. Eneo ambalo hawezi kabisa kwa sasa kufanya kitu ambacho siku za nyuma alikuwa anafanya.

Hawezi kutengeneza nafasi nyingi za magoli, hawezi kufunga sana kwa sababu tu anachezeshwa eneo ambalo siyo sahihi kwake.

Eneo la chini kabisa , eneo la kiungo mzuiaji. Kwa sasa ana kazi moja tu . Nayo ni kuilinda ngome ya ulinzi ya Yanga. Ameachana na jukumu lake kubwa lililomkuza la kuwalisha washambuliaji wa Yanga

Hana uhuru tena wa kutengeneza nafasi nyingi za magoli kama awali , hafungi magoli mengi kama awali. Hiki ndicho kinachoumiza kwa sasa. Kupoteza kiungo bora wa kushambulia na tumepewa kiungo wa kawaida wa kuzuia.

Haya yote kayafanya Mwinyi Zahera , Mwingi Zahera ambaye Leo hii anampeleka kwenye kaburi lile lile alilopo Fei Toto. Leo hii Mapinduzi Balama anachezeshwa katika eneo ambalo siyo lake

Huyu ni kiungo wa kushambulia wa kati. Lakini tangu aje Yanga anachezeshwa nafasi ambazo siyo zake. Awali alikuwa anachezeshwa kama kiungo wa pembeni.

Nafasi ambayo ilikuwa ngumu kwake. Katika mchezo dhidi ya Zesco akachezeshwa kama beki wa kulia. Taratibu anabadilishwa majukumu yake ya kimsingi. Majukumu ambayo yanamfanya asifanye vizuri kama alivyokuwa Alliance FC

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x