Stori

Banda: Simba ni Ushindi Tuu Haina Matokeo Mengine

Sambaza....

Mlinzi wa zamani wa klabu ya Simba na Coastal Union  Abdi Banda anaecheza soka la kulipwa nchini Afrika Kusini amesema ukicheza Simba hakuna namna timu itafungwa na viongozi wakakubali.

Banda akiongea katika kipindi cha redio cha Mjini Fm anasema amekaa klabu hiyo kwa muda alioitumikia na kugundua hilo. “Nakumbuka tulicheza mchezo wa kirafiki wakati tupo South Afrika wakati wa maandalizi ya msimu, ile mechi Ivo Mapunda alikua kaumia na akakaa golini Manyika na tukafungwa.”

“Nakumbuma alisimama “Manice” Awadhi Juma akasema viongozi mpira una matokeo matatu hakumaliza, marehemu Hans Pope alisimama na kumwambia Simba ina matokeo moja tu haina matokeo mengine sijui kufungwa wala sare. Timu ipo hapa kuwapa furaha mashabiki wake,” alisema Banda.

Abdi Banda [jezi namba 4] akiitumikia Chippa United.
Abdi Banda pia amezima maneno yaliyokuwa yakiongelewa kuhusu mahusiano yake na klabu yake ya zamani ya Simba kwamba hakua na mahusiano nao mazuri kutokana na sakata lake la usajili alipokua anatimkia Afrika Kusini kwa mara ya kwanza kucheza soka la kulipwa.

“Mimi siwezi kukaa na kuisema Simba vibaya kwasababu ipo kwenye profile yangu, si Simba tuu hata Coastal Union ni timu ambazo nimezipitia na zimenifikisha hapa nilipo mpaka nacheza South Africa,” alisema na kuongeza

“Simba imenisaidia sana katika maisha yangu kipindi hata wakati naondoka. Nakumbuka hata yule Dewji (Kassim) kwasasa hayupo sana mbele na timu lakini ni watu wazuri sana siwezi kuelezea yote lakini siwezi kukaa kuiongelea vibaya Simba kwasababu labda ya ubaya wa mtu mmoja.”

Abdi Banda.

Banda ambae kwasasa anaitumikia klabu ya Chippa United ya Afrika Kusini amegusia nafasi yake katika timu ya Taifa huku ikionekana mara kwa mara kukosa nafasi ya kuitumikia timu hiyo licha ya kiwango kizuri anachokionyesha.

Abdi Banda “Nafasi yangu naiona timu ya Taifa na ndio maana kila siku nafanya mazoezi na nacheza katika klabu yangu nikiwa natamani namimi niwepo timu ya Taifa. Matakwa ni ya mwalimu na falsafa ya mwalim ndio itakayoamua.”

 

Sambaza....