Ramadhani Kabwili
Blog

Kuipa ubingwa Yanga ni kupingana na Ulimwengu…

Sambaza....


Ukiutazama msimamo wa ligi utagundua kuwa, Simba, Yanga na Azam ndizo timu zinazonasabishwa na ubingwa kwa ukaribu zaidi lakini, soka lina kanuni ambazo hazikaririki.

Mambo yapo hivi, Yanga yupo kileleni akiwa na jumla ya alama 80, akicheza mechi  34, Simba iko nafasi ya pili ikijikusanyia  78  katika michezo 30 Aliyocheza, na Azam katika nafasi ya tatu ikiwa na alama 67 katika michezo 34 iliyocheza.

Kwa takwimu hizi, maana yake Yanga na Azam wamealiwa na michezo minne kwa kila mmoja ili kumaliza ligi, huku Simba ikisaliwa na mechi  8 mkononi. Kwa sasa, Ili Azam achukue ubingwa ni lazima ashinde mechi zake zote zilizosalia, huku akiwaombea Simba na Yanga wafungwe mechi zao zote, kitu ambacho hakiwezekani.

Kwakuwa haiwezekani, basi Azam FC tunawatupiulia mbali katika mbio za ubingwa wa ligi kuu msimu huu.

Timu mbili zilizosalia katika mbio hizi ni Simba na Yanga. Yanga akimzidi Simba kwa alama 2 na akicheza mechi 4 zaidi akijikusanyia  alama 80 na akisaliwa na michezo Minne. Kama Simba atashinda mechi zake zote atakuwa anamzidi Yanga kwa alama 10 yaani Yanga akishinda mechi zake nne zilizosalia atakuwa na alama 92, Simba akiwa na alama 102.

Kimahesabu, ili Yanga awe bingwa sharti ashinde mechi zake nne zilizosalia, kisha Simba apoteze michezo Mitatu, na sare mbili au apoteze michezo minne kati ya Nane iliyosalia.

Msimamo wa sasa

PosTimuPWDLGDPts
1Simba SC3829636293
2Yanga SC3827562986
3Azam FC38211253375
4KMC FC38131691555

Swali, Je inawezekana kwa Yanga kupata ushindi katika mechi zake zote 4 zilizosalia? Je inawekana kwa Simba kupoteza michezo Minne, au mitatu na sare mbili?

Mashabiki wa Yanga katila moja ya mechi za Ligi Kuu Bara

Simba kwa sasa wanatakiwa kukusanya alama 15 pekee ili kutangaza ubingwa lakini alama hizo zinaweza kupungua zaidi kulingana na maendeleo ya Yanga.. Yaani mara tu Yanga itakapopoteza mchezo, itawapunguzia Simba alama 3 kati ya 15.

Naamini kuwa Simba itabeba ubingwa, na kuna sababu kuu 5 kwanini naipa nafasi Simba kubeba ubingwa kwa mara nyingine tena .

Kwanza ni ubora wa kikosi chake. Licha ya kubanwa na ratiba, lakini Simba wameonesha ukomavu mkubwa, na kuleta dhana ya kikosi kipana katika uhalisia. Kwa mfano katika mechi dhidi ya JKT Tanzania, mabadiliko ndiyo yaliyoteza faida kwa dakika za mwishoni.

Kocha Patrick Aussems anajitahidi kuwatumia wachezaji wake katika mzunguuko ambao hautowafanya wachoke sana. Na kwa bahati nzuri kila mchezaji akipewa majukumu huhakikisha haitendei makosa nafasi hiyo.

Aussems, kocha mkuu

Morali hii ya wachezaji inawafanya wawe na muendelezo mzuri wa matokeo katika kila mchezo. Moto huu usipozimika, Simba watakuwa mabingwa tena.

Sababu ya pili ni Malengo ya Timu. Simba imekuwa ikijinasibu na malengo yake ya kutetea ubingwa wa ligi kuu Tanzania bara msimu huu. Na inavyoonekana ni kweli amejiandaa kufanya hivyo.

Klabu imetulia haina changamoto nyingi za kifedha ukilinganisha na washindani wao. Hii inawapa nafasi kutimiza malengo yao bila kizuizi chochote. Haya yamekuwa yakisemwa na msemaji wa klabu hiyo Haji Manara na Mwekezaji Mkuu, Mo Dewji. Bila shaka kwa hili wamefanikiwa.

Tatu ni Mashabiki. Ni furaha kuwa kwa wachezaji na timu kwa ujumla kuwa na mahabiki wanaoujaza uwanja wakihanikiza, hii huleta morali kwa wachezaji na benchi la ufundi.

Ni mara kadhaa kwa makocha wa Simba na wachezaji kushukuru uwepo wa mashabiki wa Simba popote Tanzania. Bila shaka utakubaliana name kuwa, Simba popote pale itakapocheza Tanzania, itaingiza idadi kubwa ya Mashabiki kuliko hata timu mwenyeji. Na hii ndio chachu kubwa kwa Simba kupata ushindi kwa namna yoyote ile.

Nne, uwekezaji na motisha. Klabu yenye nia ya kubebwa ubingwa utaibaini mapema tu, tena kuanzia hatua ya usajili. Simba imefanya usajili mzuri kiasi cha kuwa na wachezaji wazuri katika kila idara.

Simba chini ya mfumo mpya wa hisa, inaonekana kuendana na soka la dunia kimfumo. Mwekezaji mkuu wa timu hiyo amekuwa ni motisha tosha kwa klabu na wachezaji kuhakikisha wanafanya vizuri katika kila mchezo, hii ni kutokana na malupulupu wanayopata wachezaji kwa kila mechi.

Uwekezaji mzuri ndio unaowafanya Simba kulisusa basi lao kwa mechi za mikoani,  hii hupunguza uchovu wa safari kwa wachezaji na benchi la ufundi. Uwekezaji unaifanya Klabu ijue kesho yake. Yaani inaweza kuwa na malengo ya muda mfupi na mrefu na mambo yakaenda sawa.. hii ni tofauti na vilabu vingine visisvyojua hata mwezi ujao vitawalipaje wachezaji wake.

Tano ni Mechi zilizosalia.

Simba imesaliwa na mechi dhidi ya  Coastal Union (Nyumbani), Kagera Sugar(Nyumbani), Azam (Nyumbani), Mtibwa Sugar (Nyumbani), Ndanda (Nyumbani), Singida United  ( ugenini), Biashara United (Nyumbani),  na Mtibwa Sugar ( ugenini).

Katika mechi hizo zote, Simba itakuwa nyumbani kwa mechi 6 na Ugenini kwa  mechi 2.

Mechi ambazo zinaonekana ngumu ni mechi dhidi ya timu zinazopambana kutoshuka daraja na zile zinazogombania ubingwa. Katika Orodha ya michezo yake iliyosalia, timu ngumu zinazoweza kumpa shida mnyama ni dhidi ya Biashara na Kagera ambazo zote zipo mkiani.

Kama mwalimu atafanikiwa vizuri katika kufanya “Rotation” ya wachezaji, Simba iatafanikiwa kuzipata alama 15 na kutangaza ubingwa.

Kwa maana hiyo Simba itatangaza ubingwa katika mechi dhidi ya Ndanda, uwanja wa taifa au dhidi ya Singida United pale Namfua, lakini hayo yote yatakuja endapo Yanga atashinda mechi zake zote za ligi.

Sambaza....
Subscribe
Notify of

0 Maoni
Inline Feedbacks
Tazama Maoni Yote
0
Tungependa kupata maoni yako, tafadhali tuambiax
()
x