Blog

Yanga wanapenda sana Hesabu za kutoa !

Sambaza....

Ndiyo hesabu pendwa kwao na wanajivunia nazo kuwa nazo. Daftari Lao limepambwa na hesabu hizi . Hata ukifungua ukurasa wa kwanza wa daftari Lao utakutana na hesabu hizi za kutoa.

Ukurasa ambao mashabiki wa Yanga walikuwa hawapendezwi na uwepo wa Dismass Ten kama msemaji wao mkuu wa klabu , huyu mdomo wake ulikuwa mfupi sana.

Ndicho kitu kilichomponza. Kila walipokuwa wanatazama nyuma walikuwa wanakutana na taswira ya Jerry Muro , huyu alikuwa na mdomo mrefu haswaa, aliwafanya Yanga watambe ambaye kwa kipindi hicho hakuwepo.

Na walipotazama kulia walikutana na Haji Manara huyu aliwafanya Yanga wawe wanyonge sana . Alikosekana mtu wa kupambana na Haji Manara hii ilikuwa kwa mujibu wao.

Wakaamua kumtoa Dismass Ten , tena wakati wanafanya hesabu za kutoa kwa Dismass Ten walidai kuwa anachangia mashabiki kutokuja uwanjani kwa wingi , Dismass akatolewa rasmi.

Ili kushindana na Haji Manara wakamweka Hassan Bumbuli na Antonio Nugaz , Antonio Nugaz akawekwa kama mtu wa kumtoa Haji Manara kwenye reli , akafundishwa mbinu zote za kumtoa Haji Manara kwenye reli.

Swali likabaki baada ya kumtoa Dismass Ten mashabiki wanahudhulia kwa wingi kwenye mechi ?. Tuachane na hilo turudi kwenye hesabu za Juma Balinya na Yikpe.

Hapa tena kulifanyika hesabu ya kutoa , Alitoka Juma Balinya ili Yikpe apate nafasi kwenye kikosi cha Yanga . Tulitegemea Yikpe atakuwa mmoja wa wachezaji bora kusajiliwa na Yanga Lakini ikawa tofauti kabisa.

Yikpe

Hana ubora mkubwa wa kumzidi Juma Balinya , Juma Balinya ni moja ya wachezaji bora ambao kwa sasa wanakosekana kwenye kikosi cha Yanga. Yanga kwa sasa inahaha sana kufunga magoli kwa sababu hawana mshambuliaji ambaye angehusika kwenye kufunga magoli.

Mshambuliaji ambaye angewasaidia kwa kiasi kikubwa ni Juma Balinya ambaye muda huu ameshamaliza kufanyiwa hesabu za kutoa. Hayupo tena, mashabiki wanalia na Yikpe .

Mhamasishaji wa Yanga naye anajibizana hadharani na mashabiki wake , mashabiki ambao ni wateja . Wateja ambao wanategemewa kuja kununua bidhaa ya Yanga Lakini wanajibiwa vibaya na mhamasishaji tena hadharani na hii ni kwa sababu Yanga inapenda sana hesabu za kutoa, wako tayari kumtoa mteja asiwe mteja tena!.

Sambaza....