Ligi Kuu

Tunamuua Mapinduzi Balama kumchezesha Pembeni

Sambaza....

Kuna vipaji vingi sana Tanzania ambavyo vinacheza eneo ambalo siyo sahihi. Eneo ambalo mara nyingi huwafanya wachezaji husika kutokuwa huru kucheza kwenye eneo hilo.

Unajua kinachotokea kipindi wanapokuwa hawapo huru kucheza eneo hilo ?. Mchezaji anaposhindwa kuwa huru kucheza eneo ambalo siyo sahihi na eneo lake halisi kiuchezaji hushindwa kuzalisha kitu bora.

Uzalishaji wake uwanjani huwa ni wa kiwango cha kawaida ukilinganisha na kipindi ambacho yeye angechezeshwa eneo lake halisi. Eneo ambalo kila uchwao analijua zaidi.

Eneo ambalo majukumu yake siyo mapya ukilinganisha na eneo jipya ambapo ataenda kukumbana na majukumu mapya ambayo awali hakuwa ameyazoea kukumbana nayo.

Inawezekana hapa kuna mtu anaweza kusema kuwa mchezaji anatakiwa awe tayari kucheza eneo lolote ndani ya uwanja kulingana na matakwa ya kocha.

Kitu ambacho ni kweli , lakini kiwango chake hakitokuwa maradufu kama ambavyo angecheza eneo lake husika. Atakuwa na makosa mengi binafsi kwa sababu ya kutimiza majukumu mapya kwa wakati huo.

Ilianza kwa Faisal Salum “Fei Toto” ambaye alitolewa eneo lake halisi la kiungo cha juu na kushushwa mpaka eneo la kiungo mkabaji. Eneo ambalo alicheza kwa makosa mengi.

Eneo ambalo lilimfanya afanye rafu nyingi sana ambazo kwa wakati mwingine zilikuwa hazina lazima. Leo hii Fei Toto anahangaika kuingia kwenye kikosi cha Yanga , kitu ambacho namuombea afanikishe.

 

Feisal Toto

Tumetoka kwa Fei Toto tumerudi kwa Mapinduzi Balama. Huyu kiuhalisia ni kiungo wa kati. Lakini amekuwa akibadilishwa majukumu sana.

Mechi ya jana dhidi ya Kagera Sugar , Mapinduzi Balama alicheza kama winger wa kulia. Eneo ambalo hakuwa na uwezo mkubwa sana ukilinganisha na eneo la kiungo cha Kati eneo ambalo amelizoea.

Hakuwa na Kasi kubwa ambayo winga wa pembeni anatakiwa kuwa nayo. Hakuwa na uwezo wa kupiga krosi nyingi kumlisha Ditram Nchimbi.

Balama Mapinduzi akiachia fataki na kufungs bao la kwanza kwa Yanga

Eneo hili limeficha sana uwezo wake halisi. Uwezo ambao alitakiwa auoneshe kwenye dimba la Kati, apige pasi nyingi , atengeneze magoli na afunge magoli akitokea katikati ya uwanja.

Sambaza....