Ligi Kuu

KMC yaanda vita na Coastal Union.

Sambaza....

Kikosi cha Timu ya KMC FC leo kitaanza maandalizi kuelekea katika mzunguko wa pili wa michuano ya Ligi kuu ya NBC soka Tanzania Bara itakayoendelea Disemba 15 mwaka huu kwa mujibu wa ratiba ya Bodi ya ligi kuu Tanzania TPLB.

Katika hatua hiyo KMC FC itawakaribisha Coastal Union ya mkoani Tanga katika uwanja wa Uhuru hapa Jijini Dar es salaam ambapo itapigwa siku ya Alhamisi ya Disemba 15 saa 16:00 jioni.

Ibrahim Ame.

Timu hiyo ya Manispaa ya Kinondoni chini ya kocha Mkuu Thierry Hitimana itaanza maandalizi hayo leo ikiwa imetoka kupata ushindi katika mchezo hapo jana wa michuano ya kombe la Azam Sports Federation ASFC dhidi ya Tunduru Korosho uliomalizika kwa KMC FC kupata ushindi wa magoli sita kwa moja.

Aidha katika michezo hiyo ya ligi kuu ya NBC, KMC FC inajiweka vema ili kuanza vizuri katika michezo mitatu ya nyumbani kwa kuhakikisha kwamba inavuna alama zote muhimu na hivyo kuendelea kujiweka sawia katika msimamo wa Ligi.

” Tunakwenda tena kwenye mzunguko wa pili, tunafahamu kuwa utakuwa wenye ushindani zaidi ya ule wa kwanza kutokana na kwamba ndio tunakwenda kumaliza ligi , sasa kila timu itakuwa inajipanga kwa ajili ya kupata matokeo, hivyo KMC FC tunakwenda tukiwa imara na tutafanya vizuri kwenye michezo yetu,” alisema Christina Mwagala afisa habari wa KMC

“Tutakuwa na michezo mitatu ya mwanzo wa mzunguko wa pili ambapo yote tutakuwa nyumbani, michezo hiyo ni dhidi ya Coastal Union ya mkoani Tanga, Polisoi Tanzania pamoja na Simba, hivyo tuna waahidi mashabiki zetu kuwa tutafanya vizuri kwenye michezo hiyo,” aliongeza Mwagala

KMC FC ipo katika nafasi ya 10 na jumla ya alama 16 baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza na kwamba inakwenda kwenye mzunguko huo wa pili ikihitaji ushindi kwa kila mchezo ili kufanikisha kupanda kwenye nafasi nzuri mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Sambaza....